Please Limited time Offer!

Riwaya ya ‘Nguu za Jadi’ Comprehensive Study Guide

Read also Mwongozo Wa Mapambazuko ya Machweo na Hadithi Nyingine

UTANGULIZI

Mwongozo huu una nia ya kuwa mwanga gizani kwa wasomi wa riwaya ya Nguu za Jadi,, kwa kutoa maelezo maridhawa kuhusiana na hadithi iliyomo humu. Ili kufanikisha hili, mwongozo huu umeangazia masuala kadhaa katika hadithi. Kabla ya kwenda katika hadithi binafsi, ni vyema kuangazia vipengele Fulani vya diwani.

MADA: RIWAYA YA NGUU ZA JADI,.

Kuutumia Mwongozo.

Mwongozo huu umechambua kila hadithi kwa mapana na marefu. Umeangazia masuala tofauti tofauti katika hadithi zote, ili kuhakikisha kwamba maomaji anaelewa yanayoshughulikiwa kwa ubainifu wa kipekee. Masuala haya yanaanzia kwa mtiririko wa hadithi na ufaafu wa anwani hadi mitindo ya uandishi. Masuala yaliyoshughulikiwa ni pamoja na;

Dhamira ya Mwandishi.

Ni lengo la mwandishi, yaani sababu ya kuandika hadithi husika. Inaeleza ujumbe ambao mwandishi alinuia kupitisha kwa msomaji. Inaweza pia kuelezwa kama mafunzo ambayo msomaji anapata kutokana na kusoma hadithi husika. Dhamira inaweza kuwa kupitisha ujumbe kwa njia tofauti ikiwemo kuonya, kusawiri hali Fulani katika jamii au kuelimisha kuhusu suala fulani.

Maudhui

Ni masuala nyeti yanayoshughulikiwa katika hadithi. Ni mambo makuu hasa kuhusu jamii yanayoibuka kutokana na kusoma hadithi Fulani. Baadhi ya maudhui yanayojitokeza katika hadithi nyingi ni pamoja na elimu, utamaduni, mapenzi na ndoa, migogoro na migongano, uzinzi, ulaghai na unafiki, usaliti, nafasi ya mwanamke, ubabaedume na mengi mengine.

Wahusika

Ni watu au viumbe ambao wanatumiwa na mwandishi kuwasilisha ujumbe wake kwa hadhira. Katika hadithi zote, wahusika waliotumika ni binadamu, wanaoakisi jamii halisi. Wahusika hawa hutofautiana kwa hulka(sifa) kulingana na ujumbe toofauti ambao mwandishi anawatumia kupitisha. Hivyo basi, kila mhusika, wahusika wakuu na wasaidizi huwa na sifa zake na umuhimu katika hadithi.

Mbinu za Uandishi.

Ili kuleta mvuto, mwandishi hawezi kutumia lugha iliyo kavu. Lazima aifinyange lugha na kuisuka kipekee ili kuleta mnato kwa msomaji anapoanza kupitia kazi yake. Kuna aina tofauti za mitindo ya uandishi ambayo hutumika kutimiza hili.

1. ISTILAHI ZA LUGHA/ TAMATHALI ZA USEMI

Tashbihi/Tashbiha/Mshabaha. Hii ni mbinu ya kufananisha vitu viwili vyenye sifa sawa kwa kutumia vihusishi vya ulinganisho kama vile mithili ya, kama, sawasawa na, mfano wa na nyinginezo. Kwa mfano; Kamau ni mrefu mithili ya twiga.

Istiara/Sitiari. Hii ni mbinu ya kulinganisha vitu viwili vyenye sifa sawa moja kwa moja bila kutumia vihusishi vyovyote. Kwa mfano; Siku hizi amekuwa wali wa daku(yaani ameadimika, haonekani)

Tashihisi/Uhuishi/Uhaishaji. Ni mbinu ya kuvipa sifa za uhai vitu visivyo na uhai kama vile kuongea, kutangamana na kutekeleza mambo ya kibinadamu. Kwa mfano; hofu ilimkumbatia.

Methali. Ni tungo fupi zilizogawika katika sehemu mbili ambazo hubeba ujumbe wenye hekima. Huwa na maana ya juu, inayotokana na maneno yaliyotumiwa na maana ya ndani isiyohusiana na maneno hayo, ambayo huongoza matumizi yake. Kwa mfano; mla na miwili hana mwisho mwema.

Mwongozo Wa Riwaya Ya ‘Nguu za Jadi’

Semi(Misemo na Nahau). Ni tungo fupi zinaoundwa kwa kuunganisha maneno, na ambazo maana yake na matumizi huwa tofauti na maneno yaliyotumika. Kwa mfano; enda segemnege- haribika, enda kombo.

Takriri/ Uradidi. Ni mbinu ya kurudiarudia neno au fungu la maneno kwa nia ya kutilia mkazo hoja fulani au kusisitiza. Uradidi huu unawea kutumiwa na mwandishi moja kwa moja katika usimulizi au ukatumiwa na mhusika katika mazungumzo. Kwa mfano;misitu kwa misitu ya mahindi na maharagwe.

Tabaini. Ni mbinu ya kutumia ukinzani kwa nia ya kudhihirisha wingi. Aghalabu hudhihirika kwa

matumizi ya ‘si’ ya ukanushi. Kwa mfano; kila kitu kwake kilipendeza, si macho, si uso, si

mavazi, si viatu, si sauti.

Chuku. Ni matumizi ya maelezo yaliyotiliwa chumvi kwa ajili ya kuonyesha uzito wa jambo au hoja fulani, na pia kumtumbuiza msomaji. Maelezo huelezwa kwa kiasi cha kuchekesha, kwani huzua hali ambazo ni wazi haziwezekani, lakini zinazokubalika kifasihi. Kwa mfano; hasira zake zingeweza kuivunja bilauri kwa kuiangalia tu.

Balagha/Maswali Balagha. Ni mbinu ya kutumia maswali yasiyohitaji majibu, kwa kuwa aidha majibu yako wazi, hayapo au hayahitajiki. Maswali haya husaidia kuelewa fikra za mhusika, kutoa taarifa zaidi au kumchochea msomaji kuwaza zaidi. Kwa mfano; kwa nini haya yanipate mimi?

Uzungumzi Nafsia/Monolojia. Ni mbinu ambapo mhusika hujizungumzia mwenyewe aidha kwa sauti au akilini. Huwezesha msomaji kujua mawazo, maoni au mipango ya mhusika. Kwa mfano;

“Muradi haya yashatokea, sina budi kukubali,” Mercy alijisemea moyoni.

Tanakali/ Tanakali za Sauti. Ni mbinu ya kuiga milio au sauti zinazotokea katika hali tofauti za kimazingira au sauti za wanyama na vitu tofauti. Kwa mfano; kriii! Kriii! Kriii! Simu yangu ilikiriza.

Dayolojia. Ni mbinu ya kutumia mawasiliano ya moja kwa moja kati ya wahusika wawili katika usemi halisi. Mawasiliano haya huhusu mada fulani wanayochangia wote. Mbinu hii busaidia kuonyesha mkinzano wa kimawazo, migogoro, maoni gofauti ya wahusika, n.k.

Kuchanganya Ndimi/ Lugha Mseto. Hii ni mbinu ya kutumia lugha mbili tofauti katika usemi, Kiswahili na lugha nyingine. Mara nyingi, maneno kutoka lugha ya pili huandikwa kwa mtindo wa italiki. Aghalabu huwa Kiingereza lakini yaweza kuwa lugha nyingine kama lugha ya mama,

Kiarabu, n.k. kwa mfano; “Mwanao ni mzima. He’s out of danger.”

Utohozi. Ni matumizi ya maneno kutoka lugha nyingine, aghalabu Kiingereza yaliyobadilishwa muundo na matamshi kuwa ya Kiswahili. Kwa mfano. Daktari(doctor), begi(bag), ticket(tiketi),n.k

Kejeli/ Stihizai/ Dhihaka. Ni mbinu ya kutumia maneno ya kumsimanga mtu, tukio au suala fulani. Hali hii huweza kupunguza uzito wa hali au jambo au kumtilia mtu hamu ya kubadilika. Inaweza kutumiwa na mwandishi mwenyewe katika maelezo ya suala au mhusika kwa mwingine. Kwa mfano; alipata alama 10 katika hisabati. Kweli alijaribu, kama binadamu.

Nidaa. Ni mbinu ya kudhihirisha hisia za ndani kwa kutumia vihusishi na alama ya hisi(!). Kwa mfano, alifurahi sana kufika nyumbani. Popote ambapo alama hiyo imetumika, hiyo ni mbinu ya nidaa. Mtihani mkuu kwa mwanafunzi ni kufahamu hisia ambazo zinaakisiwa na alama hiyo.

Zinaweza kuwa furaha, huzuni, mshangao, mtamauko, hasira, amri, n.k. Laiti angalijua!

Koja. Ni mbinu ya kudhihirisha wingi wa vitu kwa matumizi ya koma kwa ajili ya kuorodhesha. Mbinu hii inaweza kuwasilisha kuwepo kwa lukuki ya vitu au mfuatano wa matukio mengi. Kwa mfano; Maria alifika nyumbani, akavua sare za shule, akaoga, akaenda mtoni kuchota maji, akapika, akala na kulala.

Mdokezo. Ni mbinu ya kuachia mambo yakining’inia, yaani kuacha bila kukamilisha ujumbe fulani kwa kutumia alama za dukuduku(…). Inaweza kuwa sehemu inayoweza kujazwa, itakayoelezwa mbeleni au kumwachia msomaji kujijazia. Pia inaweza kuwa zao la kukatizwa kalima wakati wa mazungumzo. Kwa mfano; aliingia ndani na kusubiri akijua wazi kuwa mgaagaa na upwa…

Tasfida. Ni mbinu ya kutumia msamiati wenye adabu ili kuepuka lugha chafu. Hutumika kuepuka lugha inayoweza kuzua hisia hasi au kutia kinyaa. Kwa mfano, mja mzito badala ya kuwa na mimba, kubaua/kutabawali au kwenda haja ndogo badala ya kukojoa.

Tadmini. Ni mbinu ya kutoa marejeleo katika misahafu(vitabu vya kidini) kama vile Biblia na Korani, na kuyahusisha na hali fulani katika kazi ya kifasihi. Kwa mfano; ukaidi haujaanza leo, ulianza na Adamu na Hawa kwenye bustani la Edeni.

Tanakuzi. Ni mbinu ya kutumia maneno yenye kinyume katika sentensi moja na kuzua kauli zenye ukinzani. Aghalabu hutumika kuonyesha hali ya utata. Kwa mfano; asali iligeuka shubiri. Alikufa na kufufuka ilipobidi.

Lahaja. Ni matumizi ya maneno ya lahaja tofauti za Kiswahili ambayo hayapo katika Kiswahili sanifu. Upekee wake ni matumizi ya maneno yasiyo ya Kiswahili sanifu bali vilugha vyake. Kwa mfano; kahawa tungu(kahawa chungu), mwananti kuivunda nti(mwananchi kuivunja nchi).

2. Mbinu za Kimtindo

Sadfa. Ni mtindo ambapo matukio mawili yanayohusiana hutukia kibahati kwa wakati mmoja, au kwa mfululizo kama kwamba yamepangwa. Matukio haya aghalabu huwa na matokeo fulani.

Kwa mfano; kukutana na msaada wakati wa tatizo bila kutarajia.

Kinaya. Ni mtindo ambapo matukio huenda kinyume na matarajio yetu, aidha kulingana na mfululizo wa awali wa matukio, au kwa kuyalinganisha na maisha halisi. Pia mbinu hii inaweza kudhihirishwa kupitia kwa usemi wa mhusika. Kwa mfano; kumpa hongera mtu aliyefeli au kusherehekea baada ya kufeli.

Majazi. Ni mtindo wa kuwapa wahusika majina kulingana na tabia au maumbile yao. Majina haya huitwa majina ya majazi/kimajazi. Kwa mfano; mtu katili anaweza kupatiwa jina ‘Kedi’.

Taswira. Mtindo wa kutoa maelezo ya ndani kuhusu suala fulani kiasi cha kujenga picha ya kile kinachorejelewa kwenye akili ya msomaji. Kuna taswira toofauti kama vile mwonekano, mnuso au harufu, hisi na mguso, kulingana na picha inayozalishwa. Kwa mfano; kaptura yake nyeusi iliyochakaa ilirembwa kwa viraka vya kila rangi, hungetambua rangi yake asilia.

Mwongozo Wa Riwaya Ya ‘Nguu za Jadi’

Taharuki. Ni mtindo wa kutoa maelezo taratibu kwa kusaza habari fulani ili kumtia msomaji hamu ya kujua zaidi. Pia huweza kumwacha msomaji akining’inia mwishoni mwa kisa na kumwacha kujijazia kuhusu masuala fulani.

Kisengerenyuma/Mbinu Rejeshi. Ni mtindo wa kurejelea matukio yaliyotukia muda uliopita, lakini yenye uhusiano na yale yanayosimuliwa. Yanaweza kurejeshwa na msimulizi au mhusika fulani kupitia kumbukumbu zake.

Kiangaza Mbele/Kisengerembele/Kionambele. Ni mtindo wa kudokeza mambo yatayotukia mbele kabla hayajatukia, na kuyahusisha na yale yanayotukia wakati huo.

Utabiri. Ni mbinu ambapo mhusika hudokeza jambo kisha likatukia baadaye bila yeye kutarajia. Tofauti yake na Kiangazambele ni kwamba utabiri huwa jambo la kukisia au kudokeza tu, bila uhakika wake wa kutokea.

Jazanda. Ni ufananisho wa mzito wa vitu viwili visivyo na uhusiano wa moja kwa moja, ambavyo hulinganishwa na kulinganuliwa kwa njia ya mafumbo. Kwa mfano, Bi. Sarafu alilalamika kuwa jembe la mumewe lilishindwa na kazi.

Ishara. Ni mambo, vitu au matukio ambayo huonekana au kutukia kabla ya jambo fulani yanayoashiria. Mambo haya huwa na uhusiano fulani na matukio yanayoashiria. Kwa mfano; milio ya bundi inayomtia mhusika wasiwasi kabla ya janga fulani kutokea.

Ritifaa. Ni mtindo ambapo mhusika aliye hai humzungumzia mhusika aliyefariki kama kwamba yuko hai na anamsikia. Huweza kuonyesha uhusiano kati yao, kueleza hisia za ukiwa au kumtakia neema.

Lakabu. Ni matumizi ya majina ya kupanga kuwarejelea wahusika. Majina haya huambatana na sifa fulani za mhusika. Tofauti na majazi ni kuwa lakabu huwa majina ya kupanga, bali si majina halisi ya wahusika.

Ushairi Nyimbo. Barua

Mwingiliano wa Vipengele.

Ni muhimu kuelewa kwamba kuna mwingiliano wa kipekee katika vipengele hivi tofauti vya hadithi, kwani haviwezi kushughulikiwa kwa ukamilifu. Baadhi ya mwingiliano ni kama ufuatao;

Dhamira ya Mwandishi na Maudhui. Dhamira ndiyo huongoza maudhui ambayo yanashughulikiwa katika hadithi. Hivyo basi, mambo haya mawili huingiliana pakubwa. Dhamira ndiyo hufungua nafasi kwa maudhui ya hadithi. Kwa mfano, iwapo mwandishi anadhamiria kudhihirisha maovu yanayotendewa wananchi na wanasiasa au viongozi, lazima kuwepo maudhui ya siasa au uongozi au yote.

Dhamira na Wahusika. Kila dhamira huwasilishwa kwa kutumia mhusika au wahusika fulani. Bila wahusika, dhamira haiwezi kutimizwa wala wahusika hawawezi kuwa na maana bila dhamira. Sifa za wahusika zinalingana na dhamira na kubwa zaidi, umuhimu wao huhusiana moja kwa moja na dhamira ambayo wanatekeleza. Kwa mfano, iwapo mwandishi anadhamiria kudhihirisha madhila ya wanawake katika jamii, lazima awepo mwanamke anayetekeleza dhima hiyo.

3. Maudhui na Wahusika.

 Maudhui huwasilishwa kupitia kwa wahusika pia. Vitendo vya wahusika ndivyo huzalishwa maudhui yanayoangaziwa katika hadithi. Hivyo basi, kuna uhusiano mkubwa kati ya sifa za wahusika na maudhui. Kwa mfano, kukiwepo na maudhui ya usaliti, lazima kuwepo mhusika msaliti, iwapo kuna maudhui ya tamaa na ubinafsi, lazima kuwepo mhusika mbinafsi na mwenye tamaa. Hivyo basi, ni vyema msomaji kuoanisha masuala haya pale ambapo hayashughulikiwa yote mawili.

Maudhui na Mtindo/Mbinu za Uandishi. Kuna pia mwingiliano wa kadri kati ya vipengele hivi. Japo si kila mara haya hutokea, baadhi ya mbinu huingiliana na Maudhui. Baadhi ya mbinu husawiri maudhui fulani. Kwa mfano, mtindo wa kinaya aghalabu huhusiana pakubwa na maudhui ya usaliti. Mbinu tofauti pia hubeba maudhui mengine kama vile dayolojia, ushairi, nyimbo, n.k.

Mtindo na Wahusika. Mitindo pia huweza kusaidia kuelewa wahusika na hulka zao zaidi. Kwa mfano, mbinu za majazi na lakabu husaidia katika kuelewa sifa za wahusika fulani. Mbinu nyingine zinazoleta haya ni kama dayolojia, kinaya, uzungumzi nafsia na nyinginezo.

Kutokana na maelezo haya, ni muhimu kutilia maanani kila ujumbe unaopatikana kwenye hadithi zote ili kuimarisha uelewa wake na pia kuwa na uwezo wa kukabiliana nazo katika mtihani.

Mwongozo Wa Riwaya Ya ‘Nguu za Jadi’

Jalada, Anwani na Muhtasari

Katika jalada la riwaya ya Nguu za Jadi, kuna vitu anuwai vinavyoonekana, na vinaweza kuwa na fasiri mbalimbali kwa wasomaji tofautitofauti. Vitu vilivyopo kwenye mchoro wa jalada hilo ni: 

  1. Picha ya mwanamume mzee anayemzungumzia mvulana. Kutokana na wanavyoonekana, ni wazi wamefunikwa kwa kiwango cha haja na giza. Hii inaweza kuchukuliwa kama ishara ya mtoto wa kiume ambaye ametanzwa na matatizo,  ambaye hajapewa hadhi anayostahili katika jamii, kama inavyoonekana baadaye kwenye riwaya yenyewe. 
  • Mbele ya picha ya mwanamume anayemzungumzia mvulana kuna uwanja usiokuwa  na mimea, pengine kutokana na uharibifu wa mazingira, jambo ambalo pia linajitokeza ndani ya riwaya. 
  • Mbele huko kuna miti ambayo imefunikwa na giza kiasi, ambayo inaweza kuchukuliwa

kuwakilisha matumaini yaliyonyimwa nafasi ya kujitokeza vizuri. 

  • Nyuma ya miti kuna mlima mkubwa ulio na vilele (nguu) ambavyo vina mwangaza  juu. Hii inaweza kuchukuliwa kuwa ishara ya matatizo (mlima) na suluhu  inayopendekezwa na mwandishi ya kukabiliana na nguu (vikwazo) za tangu jadi zinazotatiza maendeleo ya jamii.  
  • Nyuma ya mlima kuna mwanga hafifu unaojitokeza. Mwanga huu unaweza kuchukuliwa

kuwa kiwakilishi cha matumaini mapya kwamba jamii iliyokumbwa na matatizo mengi kwa muda mrefu hatimaye inapata mwanga, kama inavyofanyika kwenye riwaya Lonare anapochaguliwa kuwa mtemi, jambo linaloipa nchi ya Matuo matumaini mapya ya mabadiliko chanya.  

Ufaafu wa Anwani: Nguu za Jadi

Nguu ni vilele vya milima. Katika riwaya hii, neno hili limetumiwa kisitiari, kuwakilisha vikwazo au matatizo yanayokumba jamii inayozungumziwa. Kwa hivyo, Nguu za Jadi ni vikwazo ambavyo vimekuwepo kama desturi au kanuni za maisha, na ambavyo vinadumaza maendeleo ya jamii.  

Mifano ya vikwazo hivyo kutoka katika riwaya ni:

  • Mila ambazo zinawadunisha wanawake na kuwanyima uhuru wa kujiendeleza.  Mifumo ya uongozi mbaya inayosababisha ufisadi, ukabila, utabaka, ubinafsi, hali ya kutowajibika, ufujaji wa mali za umma, uharibifu wa mazingira, ukiukaji wa haki za watoto, ukatili na wizi wa mali ya umma.  
  • Mifumo wa ubabedume uliokolea taasubi ya kiume wenye kudhalilisha wanawake na watoto wa kike.  
  • Mila zinazomnyima mtoto wa kiume nafasi ya kujiendeleza. Mila hizi zimemtelekeza mtoto wa kiume kwa kutothamini elimu na maendeleo yake.  
  • Umaskini uliokithiri.  
  • Matumizi na ulanguzi wa dawa za kulevya.  
  • Changamoto za ndoa na ukahaba.  

Riwaya ya Nguu za Jadi kwa Muhtasari

Riwaya inapoanza, mhusika mkuu, Mangwasha, yuko na wanawe wawili, Sayore na Kajewa,  katika kanisa fulani, ambapo wanajificha. Nje ya kanisa hilo, wapo watu wengine wa kabila la Waketwa, waliokimbilia usalama hapo baada ya makao yao katika eneo la Matango  kuchomwa.  

Kuna fununu kwamba jamii ya Waketwa inafurushwa kutoka makwao kwa sababu kuna watu  fulani wanaotaka ardhi ya Matango kwa nguvu.  

Mtemi Lesulia, kiongozi wa nchi, anachukia kabila la Waketwa kwani yeyeanatoka katika kabila la Wakule. Waketwa na Wakule Wana uhasarna wa tangu jadi. Lonare, ambaye ni kiongozi wa Waketwa, ana urnaarufu mkubwa nchini. Katika uchaguzi mkuu uliopita,  alitekwa nyara na kwa namna hiyo, Mtemi Lesulia aliishia kuchaguliwa bila kupingwa.  

Mangwasha ni mwanamke mwenye bidii, na anafanya kazi ya uhasibu katika afisi ya Chifu  Mshabaha. Chifu huyu ni rafiki mkubwa wa Mtemi Lesulia, naye pia anawachukia Waketwa.  Hivyo, anapanza kuwadhulumu Waketwa, jambo ambalo Mangwasha analifahamu kutokana na kufanya kazi naye. Chifu Mshabaha pia ni rafikiye Sagilu, mzee anayetaka kumuoa Mangwasha licha ya kwamba anajua msichana huyu ana mchumba, Mrima, na wanapanga ndoa. Siku ya harusi ya Mangwasha na Mrima, Sagilu anamtuma kimada wake, Sihaba,  akiwa na bomu lililofungwa kama zawadi kwa maharusi. Kwa bahati nzuri, watu  wanamshuku na maafa aliyokusudia kufanya hayafanyiki. Sagilu anamnyemelea Mrima na kumzuga kwa kutumia pesa kiasi kwamba Mrima anaisahau familia yake, huku akimwachia Mangwasha jukumu la kuwalea wana wao wawili.  

Mwongozo Wa Riwaya Ya ‘Nguu za Jadi’

Nchi ya Matuo inakumbwa na matatizo mengi. Kuna matatizoya kiuchumi yanayosababishwa na uongozi mbaya na ufisadi uliokithiri. Mtemi Lesulia anaendeleza ubaguzi dhidi ya Waketwa na vijana wengi walio na elimu hawapati kazi za kujiendeleza kimaisha. Kwa mfano, uteuzi wa wagombea nafasi za uongozi ukiwa umekaribia, machifu  wanalazimishwa kuwahamisha Waketwa kutoka Matango ili viongozi wanaopendelewa na mtemi wasipate upinzani, na yeye Mtemi Lesulia asishindwe na mpinzani wake mkuu wa kisiasa, Lonare. Sihaba anatumwa kwenda kuhakikisha kwamba makazi ya Waketwa yameteketezwa,  

Anawatumia vijana ambao wanatumia petroli kuchoma makazi hap. Lonare na wafuasi wake wamepeleka kesi mahakamani, na akiwa na wenziwe, kama vile Ngoswe, wanawashawishi watu kurudi katika mako yao ya zamani kule Matango ambako wanajenga mahema. Hata hivyo, siku ya tatu, vijikaratasi vinasambazwa kuwataka watu watoke kwenye ardhi hiyo  ambayo, inabainika, imetwaliwa na kupewa Nanzia, mkewe  

Mtemi Lesulia, na rafikiye mtemi, Mbwashu. Hawa wanataka kujenga jengo la kibiashara katika ardhi hiyo ya Matango. Watu wanaokuja kuanza ujenzi wanafukuzwa na Waketwa walioamua kuitetea ardhi yao kwa vyovyote vile. Baada ya kuona kwamba mpango wao umetibuka, Mtemi Lesulia anamtumia Sagilu kumpa Mrima pesa nyingi pamoja na  ahadi kwamba atapewa kazi serikalini, ilimradi amfanyie Mtemi Lesulia kampeni na kuwaendea kinyume Waketwa.  

Kipindi kifupi kabla ya uteuzi wa watakaopeperusha bendera za vyama mbalimbali, Sagilu  anatofautiana na mwanawe, Mashauri, baada ya mwanawe kugundua kwamba babake ana uhusiano wa kimapenzi na mpenzi wake, Cheiya. Mtemi Lesulia naye anakosana na mwanawe, Ngoswe, wakati anapanga njama ya kuvuruga zoezi la uteuzi ili kuwaharibia wapinzani wake nafasi za kuteuliwa. Ngoswe anaona kwamba hatua ya babake inaongozwa na ubinafsi wa kujitakia uongozi na kutojali kwamba baadhi ya watu huenda wakapoteza maisha yao katika vurugu anazopanga. Sagilu anashindwa katika uteuzi na inakuwa wazi kwamba Mtemi Lesulia atakuwa na upinzani mkubwa katika uchaguzi mkuu ujao. Kwa ushawishi wake, Chifu Mshabaha anafutwa kazi na mtemi anaamua kumwondokea Sagilu  ambaye sasa anaandamwa na sheria kwa ufisadi alioendesha nchini. Awali, tunaona Mangwasha akipoteza kazi yake katika afisi ya Chifu Mshabaha kwa kujitokeza kama mpinzani wa serikali kwani anamfanyia Lonare kampeni, kando na kwamba mara zote,  hakumkubalia Sagilu ombi la kumtaka awe kimada wake. Sihaba anatiwa mbaroni kwa kuendesha biashara haramu ya ukahaba inayosababisha wasichana wengi kuharibika lakini anaachiliwa kutokana na ushawishi aliokuwa nao serikalini. Mikasa hii inawaathiri wahusika wengi vibaya.  

Sagilu anapatwa na kichaa na mkewe mtemi, Nanzia, anaugua baada ya jengo lake la kibiashara la Skyline Mall kutwaliwa. Baada ya kulazwa hospitalini kwa muda, anafariki.  

Kwa mara nyingine, Lonare anatekwa nyara kabla ya uchaguzi lakini anafaulu kutoroka na kupata matibabu. Uchaguzi mkuu unafanyika na Lonare anachaguliwa kuwa mtemi. Rafikiye Sagilu anashindwa na Mwamba anayechaguliwa kuwa mbunge wa Matango. Lonare anawahutubia wananchi wa Matuo na kuahidi kuufufua uchumi wa nchi na kukabiliana na ufisadi serikalini. Anaahidi pia kwamba serikali yake itashughulikia tatizo la ukosefu wa ajira kwa vijana na kuhakikisha kwamba pana usawa wa kijinsia, akisema kwamba Matuo  imesambaratishwa na ubabedume. Anawaomba wananchi wenzake kujiepusha na ukabila na kuwahimiza kukataa na kufichua maovu yanapofanyika nchini.

Lonare anachagua kutolipiza kisasi dhidi ya mahasidi wake wa kisiasa.  

SURA YA KWANZA

Mangwasha yuko na wanawe katika kanisa fulani ambapo yeye na watu wa kabila lake la

Waketwa wamekimbilia usalama baada ya kuchomewa nyumba zao katika mtaa wa Matango, jijini Taria. Kuna fununu zinazosema kwamba pana watu fulani waliotaka kuitwaa ardhi ya Matango kwa nguvu. Inabainika pia kwamba mjini Taria, kuna jamii mbili ambazo  ni mahasimu wa tangu jadi, Wakule na Waketwa. Mtemi Lesulia, kiongozi wa nchi, anatoka katika jamii ya Wakule na anawachukia Waketwa. Lonare ni kiongozi wa Waketwa lakini ana umaarufu mkubwa nchini kote kwani katika uchaguzi mkuu uliopita, alikuwa na sera bora zaidi. Hata hivyo, kabla ya kufanyika kwa uchaguzi, alitekwa nyara na Mtemi Lesulia kuchaguliwa bila kupingwa. Mangwasha anafanya kazi ya uhasibu katika afisi ya Chifu  Mshabaha. Anajua kwamba Chifu Mshabaha, ambaye pia anawachukia Waketwa, anafanya mpango wa kuwadhulumu Waketwa. Kwa sababu hii, anapanga kumwona kiongozi wake,  Lonare, ili kumweleza njama zinazopangwa dhidi ya watu wake.

Mwongozo Wa Riwaya Ya ‘Nguu za Jadi’

Juhudi za Mangwasha, hata hivyo, zinatatizwa na hali kwamba jamii haimthamini mwanamke, na anashangaa kama atasikilizwa. Anaamua atafanya tu alilokusudia, liwe liwalo.  

Masuala makuu yanayojitokeza katika Sura ya Kwanza

  • Uhasama wa kikabila na kisiasa unajitokeza kwani Waketwa wanabaguliwa na kupokwa haki zao za kumiliki ardhi na kuishi kwa amani. Waketwa wanalaumiwa hata kwa mambo ambayo hayako katika uwezo wa binadamu kudhibiti, kama vile maradhi sugu  yanapowashinda madaktari. Kiongozi wa Waketwa, Lonare ameepuka kifo mara nyingi,  kifo kilichopangwa na Wakule.  
  • Ukabila ulioshamiri Matuo unawafanya Waketwa wengi kuwa katika tabaka la chini,  huku wakiwa na viongozi wachache sana serikalini.  
  • Mfumo wa ubabedume unawanyima wanawake nafasi ya kujiamini kama wahusika sawa katika jamii. Mwanamke asiyekuwa na cheo au pesa hawezi kusikilizwa (uk. 8).  ✔ Ufisadi umeshamiri katika jamii. Ardhi ya Waketwa inapotwaliwa, Chifu Mshabaha anaangalia kando kwani ameshapokea mlungula (uk. 9).  
  • Maudhui ya bidii yanajitokeza kupitia kwa mhusika Mangwasha ambaye msimulizi anasema alifunzwa kuuambaa uvivu (uk. 12).  

SURA YA PILI

Mangwasha ni msichana mwenye bidii kazini, katika afisi ya Chifu Mshabaha. Anakutana na Mrima, ambaye pia ni mwenye bidii, na kuchumbiana. Wanafanya mazoea ya kwenda kula chakula katika mkahawa unaomilikiwa na Sagilu, mzee ambaye ni rafikiye Mtemi Lesulia.  Sagilu anamtaka Mangwasha kimapenzi na anapomkataa, anaweka kisasi dhidi yake. Chifu  Mshabaha pia anamchukia Mangwasha kwa kumchumbia mwanamume asiyekuwa na pesa na kumkataa rafikiye, Sagilu, ambaye ni tajiri.  

Siku ya harusi ya Mangwasha na Mrima, Sagilu anamtuma Sihaba, kimada wake, na bomu  ambalo linalipuka na kusababisha watu waliohudhuria sherehe kutawanyika. Baada ya miaka kadhaa katika ndoa na kuwa na watoto wawili, Mrima anabadilika. Anaitelekeza familia yake na kuingilia ulevi. Mangwasha anateseka sana na anapoamua kufuatilia mumewe ili ajue ni nini kilichomfanya abadilike, anagundua kwamba anapewa pesa nyingi na Sagilu, ambaye ni adui wa ndoa yao.  

Masuala makuu yanayojitokeza katika Sura ya Pili

⮚ Mangwasha, mhusika mkuu, anajitokeza kama mwanamke jasiri na aliyejikomboa kiakili.  Hathamini tamaduni zilizopitwa na wakati, kama vile kulazimishiwa ndoa kwa misingi ya mali. Kwa msingi huu, anamkataa Sagilu ambaye anatumia ushawishi wa hela kumtaka awe mwanamke wake. Yeye ni mwenye mapenzi ya dhati, haliinayomfanya kumjali mumewe na kufuatilia ili ajue ana tatizo gani linalomfanya kuingilia ulevi na kuitelekeza familia yake.  

⮚ Sagilu anasawiriwa kama mtu katili, anayehodhi bidhaa na kuziuza kwa bei za juu wakati kuna uhaba wa bidhaa hizo. Aliwahi kuagiza maziwa ya watoto ambayo yalihatarisha maisha yao. Kwa kuwa ana uhusiano wa karibu na Mtemi Lesulia, sheria hazikumfuatilia katika suala hili, ishara ya ufisadi.  

⮚ Chifu Mshabaha anajitokeza kama mbaguzi na mpyaro. Anasema kwamba Waketwa hawana akili (uk. 20).  

⮚ Ufisadi unajitokeza kwani polisi hawajishughulishi kumtia mbaroni mwanamke anayekuwa na kilipuzi kwenye harusi ya Mangwasha.  

⮚ Sagilu ana kisasi na familia ya Mangwasha. Kwa sababu hiyo, anatumia pesa ili kumtokomeza Mrima na kwa namna hiyo, kumsababishia Mangwasha na wanawe mateso.  

⮚ Taasubi ya kiume inajitokeza kupitia mhusika Mrima ambaye anamwambia Mangwasha kwamba hamzuii kuoa mke mwingine (uk. 41).  

SURA YA TATU

Waketwa ni watu wenye bidii. Hata hivyo, wengi wao wanaishia kufanya kazi duni na wanabaguliwa kwa kila hali kwani utawala wa Mtemi Lesulia ni fisadi na unaendeleza ubaguzi dhidi yao. Kuna matatizo ya kiuchumi yanayotokana na uongozi mbaya; vijana waliosoma hawana ajira na wengi wao hawasomi kutokana na umaskini uliokithiri.

Pia, kuna uharibifu wa mazingira kutokana na mapuuza na kutojali kwa serikali.  

Uhalifu pia umeongezeka na maadili kuwakimbia watu, hasa vijana. Lonare anamtembelea Mangwasha. Tunafahamu kwamba machifu wamelazimishwa kuwahamisha Waketwa kutoka Matango ili Mtemi Lesulia asipate upinzani katika eneo hilo, na Lonare asichaguliwe, kwani wafuasi wake wengi wanaishi huko. Baadaye, Sagilu anamtembelea Mangwasha usiku na kutaka kumhonga kwa pesa ili amkubali. Mangwasha anamfukuza na kukataa Pesa zake.  Usiku huo anapolala, anaota kwamba jinyama hatari linamfukuza na mbele anakokimbilia anakabiliwa na moto mkubwa. Anapoamka, anatanabahi kwamba Matango inateketezwa kwa moto na watu wanahangaika ovyo.  

Mwongozo Wa Riwaya Ya ‘Nguu za Jadi’

  1. Maudhui ya bidii na kutobagua kazi yanasisitizwa katika sura hii. Waketwa hawakuchagua kazi kama walivyofanya Wakule. Walifanya hata zile zinazofikiriwa kuwa duni (uk. 43).  
  2. Ufisadi unajitokeza kwani watu wengi, hasa wa jamii ya Wakule, wanapata kazi hata bila kuhitimu, jambo ambalo lina madhara makubwa, kama vile vifo vinavyofanyika hospitalini ambako watu wasiosomea udaktari wanaajiriwa kufanya upasuaji wa kimatibabu. Viongozi wa kijeshi pia wanatoka katika jamii ya Wakule (uk. 44).  
  3. Uchafuzi wa mazingira pia umeangaziwa. Wananchi wanaathirika kiafya kutokana na

uchafuzi wa mazingira (uk. 46).  

  • Umaskini unawafanya baadhi ya vijana kutopata elimu ya haja, huku wasichana wakipata

mimba za mapema na kukosa kuendelea na masomo (uk. 48-49).  e) Lonare anajitokeza kama kiongozi bora kwani anapigania elimu ya wasichana na anataka kuongoza Matuo si kwa sababu ya mshahara tu bali kwa kuwa anawapenda wananchi wenzake, kuonyesha kwamba yeye pia ni mzalendo.  

f) Mwandishi ametumia jazanda ya jinyama na moto. Jinyama linalomkimbiza Mangwasha ni Sagilu ambaye ni mzee asiyekuwa na maadili, nao moto ni kiangazambele cha moto unaowachomea Waketwa makazi yao huko Matango.  

Sura ya Nne

Sura hii inaanza asubuhi baada ya watu kukesha nje ya kanisa. Hii ni baada ya kufurushwa kutoka Matango. Mangwasha na Mbungulu wanakutana na wanawake wengine ambao  wanaelezea kwamba usiku walipochomewa nyumba walikutana na vijana. Hawa walikuwa na mageleni yaliyohanikiza harufu ya mafuta ya petroli. Vijana hao waliingia kwenye gari jekundu lililoendeshwa na mwanamke fulani ambaye hawakuweza kumtambua. Mkurugenzi wa ardhi mjini Taria anakuja mahali pale akiandamana na Chifu Mshabaha na mwanamke aitwaye Mbwashu. Anawaahidi watu chakula, mablanketi na mahema ya msaada. Watu  wanakasirishwa na hatua ya kuwachukulia kama wakimbizi lakini mkurugenzi huyo anasema kwamba chanzo cha moto uliowachomea makazi yao hakijulikani kisha anaondoka. Watu  wana hasira, hawataki kuishi mahali hapo; wako radhi kwenda kukita mahema huko  Matango.  

Siku ya tatu baada ya kurudi Matango, vijikaratasi vinasambazwa kuwataka Waketwa watoke sehemu hiyo. Watu wanakuja hapo kutaka kujenga ua ili kuzingira ardhi ya Matango lakini wanafukuzwa na wenyeji, ambapo Sihaba anajeruhiwa. Huyu ndiye aliyesambaza vijikaratasi vya kuwataka watu wahame eneo la Matango. Sagilu naye ameshaonywa na Mtemi Lesulia kuhakikisha kwamba jalada halisi la ardhi ya Matango halipatikani, kwani ardhi hiyo sasa ni mali ya Nanzia, mkewe mtemi, na Mbwashu.  

Baadaye, Sihaba anamtembelea Chifu Mshabaha. Anamwachia barua zenye taarifa kuhusu  jengo la kibiashara ambalo linanuiwa kujengwa Matango. Kuna barua kutoka kwa Mtemi Lesulia inayoeleza kwamba kipande hicho cha ardhi ni mali ya Nanzia na Mbwashu.  Mangwasha anazirudufisha barua zote na baadaye zinatumiwa kama ushahidi mahakamani katika kesi inayohusu ardhi ya Matango. Mwamba, mwanasheria anayewakilisha Waketwa katika kesi hiyo anashinda kesi kwa ushahidi huo. Mpango wa Mtemi Lesulia, Sagilu na Chifu Mshabaha wa kuwafurusha Waketwa kutoka kwenye ardhi ya Matango unakosa kufaulu.  

Mtemi Lesulia anapanga njama nyingine. Kupitia kwake Sagilu, wanampa Mrima pesa nyingi pamoja na ahadi ya kumpa cheo serikalini ikiwa atamfanyia kampeni Mtemi Lesulia na kuwaendea kinyume Waketwa. Mangwasha anapata pesa hizi pamoja na barua yenye ahadi alizopewa Mrima na anamtaarifu Lonare, Mwamba, Sauni na Sagura. Wanakutana na Mrima na kufanikiwa kumweleza ukweli kwamba anatumiwa tu kisiasa, na kwamba Mtemi Lesulia na Sagilu hawana mpango wowote wakumfaa. Wanakubaliana kurudisha pesa alizohongwa nazo kwa Sagilu, ambaye wanamkuta akiwa kwenye mkutano pamoja na wafuasi wake.  

⮚ Mangwasha na Lonare wanajitokeza kama wahusika waadilifu, wanarudisha pesa zilizotumiwa kama hongo kwa Sagilu kutoka kwa Mrima. Aidha, ni wenye mapenzi ya dhati kwa nchi na kwa watu wao. Wanamwokoa Mrima kutoka Majaani ambako  amedhoofikia kiafya.  

⮚ Chifu Mshabaha, Mbwashu, Sagilu, Mafamba na Mtemi Lesulia wanajitokeza kama wahusika fisadi na katili kwani hawajali athari za vitendo vyao vya kifisadi kwa wananchi. Mtemi Lesulia analinganishwa na mjusikafiri anayekula chakula cha mchwa na mchwa wenyewe. Maelezo haya yanajenga jazanda ya utawala dhalimu  unaowaangamiza wananchi wake.  

SURA YA TANO

Nchi ya Matuo inakaribia uteuzi wa viongozi. Sagilu, aliyekuwa na matumaini makubwa ya kupata uteuzi wa kugombea uongozi wa Matango anapata msururu wa mapigo. Ana uhusiano  wa kimapenzi na mpenzi wa mwanawe, Mashauri, aitwaye Cheiya. Mashauri anapogundua jambo hili anamchukia babake hata kumkana. Zaidi ya hayo, anajiunga na kundi linalomuunga mkono Lonare na Mwamba, ambao wanawania kiti cha mtemi na uongozi wa eneobunge la Matango mtawalia. Mashauri ni rafikiye Ngoswe, mwanawe Mtemi Lesulia.  Ngoswe anafahamika zaidi kama mlanguzi mkubwa wa dawa za kulevya, kando na kukusanya ushuru kutoka katika mashamba yånayomilikiwa na wazazi wake. Cheiya anatoka katika familia ya kimaskini lakini baada ya elimu yake na kukutana na Mashauri,  anakengeuka na kuanza kuhusudu pesa, na hii ndiyo sababu anashawishiwa na Sagilu kwa urahisi.  

Baada ya mtemi Lesulia kujua kwamba mwanawe Sagilu anamuunga mkono

Lonare,  anapanga njama ya kuzua vurugu wakati wa uteuzi ili Lonare asipate kuteuliwa akaishia kushindana naye. Anafanya hivi pia ili Sagilu achukue uongozi wa Matango. Ngoswe hamuungi babake mkono katika azimio lake. Anashangaa ni kwa nini babake yuko radhi watu wapoteze maisha yao ili yeye na rafiki yake watwae uongozi. Yeye pia anaasi na kujiunga na Mashauri katika kumuunga mkono Lonare.  

Baada ya uteuzi kufanyika, Sagilu anashindwa na mpinzani wake, Mwamba. Jambo hili linamuudhi Mtemi Lesulia ambaye anaamua kuacha sheria ifuate mkondo wake, kwani mara zote amekuwa akiwalinda marafiki zake dhidi ya sheria, hasa Sagilu ambaye ni fisadi mkubwa. Kufuatia hili pia, Chifu Mshabaha anafutwa kazi na waziri anayehusika na masuala ya utawala.  

Mangwasha anafutwa kazi kwa kuwa anamuunga mkono Lonare ambaye ni mpinzani wa Mtemi Lesulia. Analazimika kujiunga na mumewe katika kuendeleza biashara kwenye duka lao. Mangwasha anamwonea huruma mtoto wa kiume kwani ameishia kutelekezwa huku  jamii ikimwangazia zaidi mtoto wa kike. Hivyo, kwa msaada wa mashirika mbalimbali,  anafungua afisi mjini Taria ili kuwashughulikia vijana hao, ambao aliona wanaendelea kuangamia taratibu.  

Sihaba, ambaye anaendesha biashara ya ukahaba, anakamatwa na majengo anayoendelezea biashara hiyo yanafungwa. Miezi minne baada ya kushindwa katika uteuzi, Sagilu anapatwa na kichaa. Mkewe Mtemi Lesulia, Nanzia, naye anapatwa na msongo wa mawazo na kulazwa hospitalini, baada ya kupokonywa jengo la kibiashara la Skyline Mall. Ugonjwa wake unamsababishia kifo. Hata hivyo, kabla hajafa, anamweleza Ngoswe kwamba yeye ni mtoto  wa Sagilu, wala si mwanawe Mtemi Lesulia. Hali ya Sagilu inaendelea kuwa mbaya hospitalini. Mwishowe anamwomba mwanawe, Mashauri, msamaha kwa kumwendea kinyume. Mashauri anamsamehe. Mali ya Sagilu inatwaliwa na serikali kwani aliipata kwa njia ya ufisadi. Wakati huu pia inafahamika kwamba Cheiya alitumiwa kumtilia Lonare sumu  kwenye kinywaji chake. Anakamatwa na kupelekwa kwenye kituo cha polisi.  

  1. Suala la ukengeushi linaangaziwa katika kisa cha Sagilu na Cheiya. Sagilu kuandamana

na msichana wa umri wa Cheiya ni kuonyesha hali ya kutojiheshimu na kutojali maadili.  Cheiya, kwa upande mwingine, yuko tayari kujishusha hadhi kwa kuandama pesa.  Ukengeushi pia unajitokeza pale ambapo mmoja wa wasichana wanaofanya ukahaba kwa Sihaba anasema, za kutununulia chakula, nguo au hata vipodozi?” (uk. 142). Kauli hii inaashiria kwamba wasichana hawa wamekengeuka kiasi kwamba hawathamini kazi kama njia halali ya kujitafutia riziki.  

  • Suala la malezi mabaya pia linajitokeza katika sura hii kwani Ngoswe ni mwana

kindakindaki aliyeengwaengwa na kudekezwa kupita kiasi (uk. 122). Yeye anaendesha biashara ya kulangua dawa za kulevya na babake, Mtemi Lesulia, anamlinda kiasi kwamba hata wakuu serikalini hawawezi kumkamata (uk. 122-123). Sifa ya Sagilu kama mtu fisadi inajitokeza. Anashirikiana na mwanawe kuifisidi nchi kwa kushiriki biashara ya vipusa na meno ya ndovu, na Mashauri anaposhtakiwa, kesi zenyewe zinazimwa kabla ya kuanza (uk.

127).  

  • Hatua ya Ngoswe na Mashauri kuungana katika kumpigia kampeni Lonare inaashiria

uwezo wa vijana katika kuchangia mabadiliko chanya katika jamii.  

  • Ujasiri wa Mangwasha unaendelea kuonekana katika sura hii. Anapokabiliana na Chifu  Mshabaha baada ya kupoteza kazi yake, anamwambia chifu huyo kwamba yeye na wengine wanaotaka mabadiliko watazibomoa hisia zao za ukabila, ubinafsi na chuki (uk.  136).  
  • Tatizo la umaskini uliokithiri linawafanya watu kufanya mambo kinyume na maadili ya kijamii. Kwa mfano, baadhi ya wazazi wanawakubalia wana wao wa kike kushiriki ukahaba kama njia ya kujitafutia riziki (uk. 143).  
  • Kufutwa kazi kwa Chifu Mshabaha, kukamatwa kwa Sihaba, Nanzia kupoteza _jengo la Skyline Mall na hatimaye kufariki, na Mangwasha kuanzisha afisi ya kushughulikia mtoto wa kiume ni hatua muhimu katika ujenzi wa jamii mpya, jamii inayozingatia maadili na kuwajali watu.  
  • Kupitia mawazo ya Mangwasha, tunapata kuelewa falsafa ya mwandishi kuhusu maisha: kila mtu ni mhusika mkuu katika kisa cha maisha yake mwenyewe, na jambo la muhimu  ni mhusika huyo kuipa hadhira yake kitu cha kuwatia moyo maishani.  

SURA YA SITA

Siku chache kabla ya uchaguzi mkuu, Lonare anaripotiwa kupotea. Hata hivyo, wafuasi wake wanaamua watampigia kura, awepo au asiwepo. Hii ni licha ya Mtemi Lesulia kusema kwamba kiti cha mgombea nafasi ya mtemi katika Chama cha Ushirika kifutiliwe mbali kwani Lonare mwenyewe hayupo.  

Asubuhi ya siku ya uchaguzi mkuu, Lonare anapatikana ametupwa nje ya nyumba ya Mangwasha akiwa katika hali mahututi. Wafuasi wake waliokuwa wameishiwa na matumaini wanajitokeza kwa wingi kwenda kumpigia kura huku mwenyewe akipelekwa hospitalini.  Akiwa hospitalini, anamshauri Ngoswe kuacha biashara ya mihadarati kwani kwa kufanya hivyo, atakuwa anaokoa kizazi kizima kutoka katika maangamizi. Lonare anamshauri pia kuacha biashara nyingine haramu anazofanya na kujitanibu na mitandao inayoendesh  biashara hizo. Lonare anachaguliwa mtemi wa nchi ya Matuo. Baada ya ushindi huu,  anaihutubia nchi. Anaahidi kufufua uchumi wa nchi na kukata mirija ya ufisadi. Anaahidi pia kwamba serikali yake itashughulikia ukosefu wa ajira kwa vijana. Isitoshe, anaahidi kwamba atahakikisha kuwa kuna usawa wa kijinsia nchini huku akisema kwamba Matuo  imesambaratishwa na mfumo wa ubabedume. Anawaomba wananchi wenzake kuepuka ukabila na kufichua maovu yanapofanyika nchini. Anaamua kuwasamehe maadui wake wa kisiasa.  

Mwongozo Wa Bembea ya Maisha-Comprehensive Guide

Scroll to Top